Ticker

6/recent/ticker-posts

MCHENGERWA AIPONGEZA YANGA KWA KUTANGAZA TANZANIA KIMATAIFA



Na John Mapepele

Waziri wa Maliasili na Utalii, Mhe. Mohamed Mchengerwa amepongeza Timu ya Yanga kwa kuichakaza Kaizer Chiefs ya Afrika Kusini kwa bao moja kwa nunge katika uwanja wa Benjamin Mkapa jijini Dar es Salaam na kuendelea kuitangaza Tanzania kimataifa.

Ikumbukwe kuwa Timu ya Yanga katika msimu huu ilifika Fainali Kombe la Shirikisho Barani Afrika.


Akizungumza mara baada ya kumalizalika kwa mechi hiyo ya kirafiki katika kilele cha wiki ya (Wananchi) Yanga amezitaka Timu zote kuendelea kufanya vizuri ili kuitangaza Tanzania duniani.

Aidha ametumia tukio hili kuzipongeza Timu zote zinazofanya vizuri katika michuano ya kimataifa na ameiomba ziendelee kufanya hivyo Kwa kuwa kwa kufanya hivyo kunalitangaza Taifa duniani.


"Ni mategemeo yetu Timu ya Simba ambayo itakwenda kucheza Super Cup itafanya vizuri ili kulitangaza Taifa letu" amesisitiza Mhe. Mchengerwa

Pia amesema Wizara yake itaendelea kutoa ofa mbalimbali kwa timu yoyote inayofanya vizuri katika mashindano ya kimataifa ikiwa ni pamoja na kutembelea Hifadhi na Mbuga za wanyama kama ilivyofanya kwa timu ya Yanga.

Ametoa wito kwa watanzania kuwa na tabia ya kutembelea vivutio vya utalii katika Hifadhi za Taifa ili kufurahia urithi wa raslimali zao.


Bao la Yanga limefungwa na Mchezaji machachali Kennedy Msonda dakika moja kabla ya kumalizika kipindi cha kwanza na kuunyanyua uwanja kwa shangwe.

Msemaji wa Timu ya Yanga, Ally Kamwe amesema mchezo wa leo umeonesha jinsi Menejimenti ya Klabu hiyo ilivyofanya usajili mzuri katika msimu huu.

Amewataka wapenzi na mashabiki wa Timu hiyo kutarajia mambo makubwa zaidi katika msimu huu.

Post a Comment

0 Comments