Ticker

6/recent/ticker-posts

Wajumbe wa Kamati Wapongeza Uwekezaji Gesi Asilia Mtwara

Wajumbe wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar wameipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa uwekezaji mkubwa uliofanyika katika miundombinu ya uzalishaji, uchakataji na usafirishaji wa gesi asilia Mkoani Mtwara.

Wajumbe hao wametoa pongezi hizo leo Machi 22, 2024 wakiwa ziarani Mtwara kwa lengo la lengo kujifunza zaidi kuhusu shughuli za utafutaji, uendelezaji na uzalishaji wa mafuta na gesi asilia nchini.

Wajumbe hao wa Kamati, wakiongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Mwanaasha Khamis Juma, walitembelea miundombinu ya kuzalisha na kuchakata gesi asilia iliyopo eneo la Mnazi Bay Mtwara inayoendeshwa na kampuni ya Maurel and Prom na mitambo ya kuchakata gesi asilia inayoendeshwa na GASCO (kampuni tanzu ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania – TPDC) iliyopo eneo la Madimba Mtwara.

Mara baada ya ziara, Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Mwanaasha alisema kuwa pamoja na ziara hiyo kuongeza wigo wa uelewa kuhusu masuala ya mafuta na gesi, ziara hiyo pia imewapa kuona uwekezaji mkubwa wa miundombinu ya uzalishaji na uchakataji wa gesi asilia uliofanywa na Serikali pamoja na wawekezaji.

“Mbali na uwekezaji mkubwa uliofanyika kwa upande wa miundombinu ya uchakataji na uzalishaji, tunaipongeza Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kuongeza ushiriki wa TPDC katika Kitalu cha Mnazi Bay kutoka asilimia 20 hadi 40. Kwa hakika hili ni jambo kubwa” aliongeza Mhe. Mwanaasha.

Mhe. Mwanaasha aliambatana na wajumbe sita wa Kamati akiwemo Makamu Mwenyekiti wa Kamati hiyo pamoja na makatibu wa Kamati. Wengine walioshiriki ni Mkurugenzi wa Mamlaka ya Udhibiti, Utafutaji na Uchimbaji Zanzibar, Ndg. Adam Makame, mwakilishi wa Mkurugenzi Mkuu wa PURA, Ndg. Musa Ryoba na maafisa kutoka PURA na ZPRA.

Ugeni wa wajumbe hao kutoka Zanzibar ulipokelewa na Mkuu wa Wilaya ya Mtwara Mhe. Mwanahamisi Munkunda ambaye alimwakilisha Mkuu wa Mkoa wa Mtwara. Mhe. Munkunda alisema kuwa Mtwara imefurahi kupata ujio huo na kwamba ni matumaini kuwa wataweza kujifunza masuala mengi ya mafuta na gesi asilia kwa kuwa Mtwara ni kitovu cha masuala hayo hapa nchini.
Wajumbe wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar katika picha ya pamoja na Meneja wa Kitalu cha Mnazi Bay kutoka Kampuni ya Maurel et Prom, Bw. Lurent Jars. Wengine pichani ni viongozi na maafisa kutoka PURA na ZPRA.

Pichani ni sehemu ya Wajumbe wa Kamati ya Bajeti ya Baraza la Wawakilishi Zanzibar wakiongozwa na Mwenyekiti wa Kamati hiyo Mhe. Mwanaasha Khamis Juma (wapili kushoto) wakitembelea  mitambo ya kuchakata gesi asilia inayoendeshwa na GASCO (kampuni tanzu ya Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania – TPDC) iliyopo eneo la Madimba Mtwara katika ziara iliyofanyika Machi 22, 2024.

Post a Comment

0 Comments