Ticker

6/recent/ticker-posts

Kadio, Nyenza wang’ara raundi 18 za kwanza mashindano ya gofu kumuenzi Lina Morogoro

Na Mwandishi Wetu, Morogoro

WACHEZAJI wa kulipwa wa gofu kutoka Dar es Salaam, Bryson Nyenza na Hassan Kadio waliibuka vinara wa raundi 18 za kwanza za mashindano ya gofu ya kumuenzi mchezaji wa zamani timu ya wanawake Lina, baada ya kuongoza kwa kwa mkwaju mmoja.

Wote wawili walimaliza raundi 18 ya awali kwa mikwaju 73 kila mmoja , yaani mkwaju mmoja zaidi ya mshindi wa pili Nuru Mollel aliyepiga mikwaju 74.

“Mchezo bado ni mgumu ingawa nimeweza kuongoza siku ya ufunguzi kwa sababu bado kuna raundi nyingine 54 mbele yetu,” alisema Nyenza baada ya kumaliza raundi 18 za kwanza katika viwanja vya gofu mjini Morogoro jana.

Licha ya kuwa nyuma kwa mkwaju mmoja, Mollel, bado ana imani ya kufanya vizuri katika raundi tatu zilizobaki ili kumaliza mashimo 54 yaliyobaki.

Mollel aliyeshinda raundi ya kwanza katika viwanja vya TPC Golf mkoani Kilimanjaro mwezi February, bado ana imani ya kushinda pia katika michuano ya Morogoro.

“Nina uzoefu wa kutosha na fimbo mmoja si kitu kikubwa nafikiri nitakuwa vizuri zaidi katika mashimo 54 yaliyobaki,” alisema Mollel.

Mambo hayakuwa mazuri kwa Angel Eaton,mchezaji wa kike pekee wa kulipwa katika mashindano hayo baada kupiga mikwaju 84.

“ Matokeo ya leo si mazuri, lakini naweza kupata matokeo mazuri zaidi katika raundi zinazofuata. Nitapambana hadi kushinda azma hii,” alisema Eaton

Lina GP Tour ni mfululizo wa mchuano ya gofu mahsusi kwa ajili ya kumuenzi Lina Said Nkya ambaye alikuwa Mama Mlezi wa Golf ya Wanawake nchini Tanzania.

Mashindano haya yatachezwa katika viwanja vitano tofauti nchini Tanzania.Ni mashindano yanayojumuisha wacheza gofu wa kulipwa na wa ridhaa walio na viwango bora yaani Pro-Am.

“Familia ya wanagofu ilineemeka sana na Lina Nkya kwani mchango wake hausemeki,” alisema Ayne Magombe mmoja wa wachezaji wa timu ya taifa ya gofu ya wanawake nchini.

Post a Comment

0 Comments